JAMII YAKUMBUSHWA KULINDA MAZINGIRA KUEPUKA MAGONJWA YA MLIPUKO




Na. Mwandishi wetu

Mratibu wa Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Bi. Numpe Mwambenja ameikumbusha jamii kuendelea kulinda mazingira ili kuepuka uwezekano wa kukumbwa na magonjwa ya milipuko ikiwemo kipindupindu.

Ameyasema hayo wakati akifungua semina kuhusu ya masuala ya menejimenti ya maafa kwa Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii (CHW) katika Kata ya Kirumba Manispaa ya Ilemela Mkoani Mwanza, katika kuelekea Siku ya Kimataifa ya Kupunguza Maafa Dunia Oktoba 13, 2024 ambapo Kitaifa mwaka huu yanaadhimishwa Mkoani Mwanza yakiwa na kauli mbiu isemayo “Elimu ni Msingi katika Kulinda na Kuwawezesha Vijana kwa Mustakabali wa Baadae usio na Maafa”.

Kwa upande wake Mratibu wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kwa Maendeleo kutoka Shirika lisilo la Kiserikali la ActionAid Bw. Tema Hassan amesema masuala ya kukabiliana na maafa yanahitaji elimu mahususi huku akisisitiza matumizi ya teknolojia ya kisasa ili kuifikia jamii iliyokusudiwa .

“Teknolojia ni muhimu katika kuifikia jamii kiurahisi , hivyo ni vyema kuwekeza katika matumizi ya simu na mifumo ya kisasa kwa kuzingatia makundi yanayokusudiwa,” alisema Temu

Kufuatia hatua hiyo Bw.Temu amesema kuwa Shirika la ActioAid litaendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika kukabiliana na maafa nchini kwa kuzingatia unyeti wa masuala hayo na kuhakikisha jamii inaendelea kuwa stahimilivu katika masuala ya maafa.

Kwa upande wake Afisa Afya wa Kata ya Kirumba Bi. Veronica Massawe amesema usafi wa mazingira ni jambo lisiloepukika huku akiitaka jamii kuzingatia maelekezo yanayotolewa na wataalamu ili kujikinga na magonjwa ya milipuko.

“Ni muhimu kulinda afya zetu kwani, Afya ndiyo mtaji wetu sote" amesisitiza Bi. Veronica Massawe.

Ameongeza kuwa " Tumejiandaa, kukabiliana na maafa ikiwa na pamoja na kujiepusha na mazingira hatarishi yanayoweza kutuletea maafa katika kata yetu, usafi ni wajibu wa msingi kuwa na vyoo bora na kuvitumia katika kupambana na magonjwa ya mlipuko"

Naye Mwenyekiti wa Wahudumu wa Afya ya Jamii Kata ya Kirumba Bw. Wilfred Roman amesema watatumjia elimu waliyopewa katika semina hiyo kwa kuwaelimisha wahudumu wa afya ngazi ya jamii kwa kufanya afya shirikishi.

“Elimu tuliyopewa katika semina ni nyenzo muhimu tutakayoitumia katika kupambana na magonjwa ya mlipuko,” amesema Wilfred.




















Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post