KAMATI YA BUNGE YATEMBELEA OFISI ZA TBS BANDARINI DAR


Na Mwandishi Wetu

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda na Biashara, Kilimo na Mifungo imempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa alioufanya kwenye Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kwa lengo kuhakikisha usalama wa bidhaa ambazo zinatumiwa na Watanzania.

Mbali na kupongezwa uwekezaji uliofanywa kwenye shirika hilo, Kamati hiyo pia ilimpongeza Rais Samia kwa uwekezaji wa aina hiyo ambao Serikali imeufanya kwenye taasisi za Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) na Tume ya Ushindani Tanzania (TCC).

Pongezi hizo zilitolewa juzi (Oktoba 7) na Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mariam Ditopile, wakati wabunge wa kamati hiyo walipotembelea na kukagua utekelezaji wa majukumu ya taasisi tatu ambazo zipo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara za TBS, WMA na FCC.

Ditopile alisema taasisi hizo ni muhimu sana kwa kuhakikisha usalama wa bidhaa ambazo zinatumiwa na Watanzania, lakini pia kuhakikisha kuna usawa kwenye mazingira ya biashara na uwekezaji.

"Rais Samia amepiga hatua kubwa sana kupitia Serikali yake amehamasisha uwekezaji wa viwanda vya bidhaa mbalimbali ndani ya nchi, kwa hiyo kwa kuwezesha taasisi hizo zinaenda kuwahakikishia wale waliowekeza fedha zao nchini kuwa bidhaa zao zitapata soko la uhakika kwa kuzuia mianya inayoruhusu bidhaa ambazo hazina ubora au za bandia kuingia kwenye soko la Tanzania," alisema Ditopile.

Alipongeza wakuu wa taasisi hizo tatu akisema Kamati imeridhishwa na taarifa za utekelezaji majukumu za taasisi hizo na kwamba wametembelea bandarini wameona mabadiliko sasa kutokana na uwekezaji kwenye bandari.

"Lakini kikubwa ambacho tunaomba kwenye taasisi hizi zote ambazo zinashirikiana ndani ya Serikali zikiongozwa na bandari kupitia TRA, zikae pamoja ili tuongoze watumiaji wa bandari yetu ili ikachochee uchumi wa nchi yetu, lakini na kuzalisha ajira nyingi," alisema Ditopile.

"Tunataka kupunguza muda wa mzingo kuingia na kutoka na kumfikia mlaji hapo, ndipo itatuhakikishia uwekezaji wetu kuwa utaleta mantiki," alisema Mariam.

Alihimiza taasisi hizo zote zikae ni mwekezaji Bandarini DP World ili kuhakikisha kwenye mifumo yote wanasomeka na kila mmoja kama anahitaji uwekezaji wa ziada wa teknolojia ili waweze kusomana na kufanyakazi kwa pamoja na kupunguza adha ambazo wateja wa bandari wanazipata ili waweze kupunguziwa muda na usumbufu.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Exaud Kigahe, alisisitiza kuwa urasimu utakapoondolewa bandarini na mipakani itachochea na kuvutia mataifa mengine kutumia Bandari zinazopatikana nchini

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post