MWENYEKITI RAJAB ATOA MILIONI 50 KUENDELEZA UKARABATI UWANJA WA CCM MKWAKWANI


 Na Hadija Bagasha Tanga, 

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga Rajab Abrahman Abdallah ametoa kiasi cha shilingi miloni 50 kwajili ya kuendeleza ukarabati katika uwanja wa CCM Mkwakwani katika kipindi ambacho shirikisho la mpira wa miguu nchini (TFF) limepanga kuviimarisha viwanja vya Mikoani ili viweze kutumika na timu ya Taifa kwa michezo ya kimataifa. 

Mwenyekiti Rajab ametoa taarifa hiyo Jijini Tanga wakati walipotembelea na kukabidhi fedha kiasi cha shilingi milioni 50 kwajili ya kuendeleza ukarabati katika Uwanja huo uliofungwa kwa muda kwa ajili ya kufanyiwa ukarabati mkubwa. 

"Bado hapa kazi ni kubwa inaendelea na inahitaji fedha nikasema wenzetu wa TFF wameonyesha njia wamefanya kiasi walichoweza na wataendelea nikasema na mimi Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi Mkoa Tanga nije nikikabidhi chama cha mapinduzi Mkoa Tanga kiasi cha milioni 50 ili kuendeleza ukarabati, "alisema Rajab. 

"Tuishukuru Serikali katika Mkoa wetu wa Tanga kwa namna ambavyo wamepanga kutuunga mkono kwenye suala zima la kuendeleza ujenzi na ukarabati katika uwanja wetu huu wa ccm Mkwakwani, "alibainisha Mwenyekiti Rajab. 

Rais wa TFF Wallace Karia amemweleza Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga Rajabu Abdarahman Abdallah kuwa ukarabati unaofanyika kwenye Uwanja huo lengo lake ni kuuongezea hadhi ili kutumika na timu ya Taifa kwa Michezo ya Kitaifa badala ya Dar es salaam peke yake. 

"Nia yetu sisi mashindano ya kimataifa timu ya Taifa kwa mara ya kwanza katika historia ije ichezwe Tanga hapa lakini sio Tanga tuu tunarekebisha viwanja vya Mwanza,  Arusha,  Dodoma na Morogoro kuhakikisha angalau timu ya Taifa sasa ivi icheze kwenye Mikoa yote ili watanzania waweze kushangilia timu yao, alisisitiza Rais TFF. 

Akizungumza kwaniaba ya Mkuu wa Mkoa Balozi Dkt. Batilda Buriani,  Mkuu wa Wilaya ya Tanga Jafari Kubecha ameahidi kuendelea kushirikiana na chama ambacho kinatekeleza Ilani kufanya kila watakachodlekezwa huku Mstahiki Meya wa jiji Tanga Abdulrahman Shiloo akiahidi Halmashauri yake kuchangia kiasi ch shilingi milioni 30 kufanikisha ukarabati huo unaoendelea.

"Tutahakikisha uwanja wetu unakuwa ni miongoni mwa viwanja bora kabisa sio tu kwa ukanda wa Kaskazini lakini kwa ukanda bora nchini na tunakuahidi kwamba tunashirikiana na chama kuhakikisha uwanja wetu unakamilika kwa wakati na unakuwa bora, "alisisitiza Kubecha. 

Mikoa itakayoguswa ni Mwanza, Arusha,  Dodoma na Morogoro na Tanga katika hatua ya awali ambapo ameziomba Halmashauri Nchini kuchangia katika uboreshaji wa viwanja hivyo huku akipongeza juhudi za Mwenyekiti wa ccm Mkoa Tanga kwa kusaidia michezo katika Mkoa huo. 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post