OUT YATOA MAFUNZO KUIMARISHA UFUATILIAJI NA USIMAMIZI WA MIRADI SERIKALINI


Mafunzo ya ufuatiliaji na tathmini yanayoendeshwa na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kwa watumishi wa mamlaka za serikali za mitaa pamoja tawala za mikoa yanatarajiwa kuimarisha usimamizi pamoja na ufuatiliaji wa maendeleo ya miradi inayowekezwa na serikali katika kupeleka shughuli za maendeleo kwa wananchi kwa kuwa watumishi katika idara hizo watakuwa wameimarika vyema.

Rai hiyo imetolewa na Kaimu Mkurugenzi kitengo cha Ufuatiliaji na Tathimini, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Ndg. Mussa Otieno, wakati akifungua mafunzo ya awamu ya pili ya Ufuatiliaji na Tathmini akimuwakilisha Katibu Mkuu OR-TAMISEMI Mh. Adolf Ndunguru, jijini Dodoma.

“Serikali inatumia bajeti kubwa katika mamlaka za serikali za mitaa, baada ya mafunzo haya tunaamini kila mmoja atakuwa ameimarika na atakuwa na uwezo wa kutimiza malengo yanayotakiwa katika maswala ya ufuatiliaji na tathmini ili miradi ya serikali iendane na malengo yaliyopangwa. Tukatumie vyema utaalam tutaopata hapa na tukawashirikishe na wenzetu tunaofanya nao kazi pamoja ili kuwa na timu nzuri kwa ajili ya kuimarisha ufuatiliaji na tathmini katika halmashauri tunazotoka,” amesema Ndg. Otieno.

Aidha, Mkurugenzi wa Idara ya Ufuatiliaji na Tathmini wa Utendaji wa serikali, ofisi ya Waziri Mkuu, Bi. Sakina Mwinyimkuu, amesema serikali za mitaa ndiyo mtekelezaji mkubwa wa shughuli za serikali, karibu 70% ya shughuli zote za serikali zinatekelezwa na mamlaka ya serikali za mitaa hivyo washiriki wa mafunzo haya ya ufuatiliaji na tathmini wanatarajiwa kuiongezea uwezo serikali kufikia malengo yake ya kitaifa ikiwemo dira ya maendeleo.

“Chuo Kikuu Huria cha Tanzania ni mdau anayetusaidia kujengea uwezo taasisi za umma katika ufuatiliaji na tathmini, serikali za mitaa ndiyo watekelezaji wa shughuli za serikali na ndiyo wanaotoa picha ya utendaji wa serikali kwa jamii. Hili ni eneo linaloweza kuwabadilisha mitizamo ya wananchi na kuwajengea imani kwa serikali yao kwa kuona inasimamia vyema utekelezaji wa sera, miradi na mipango. Hivyo mafunzo haya yatawasidia simamia vyema utekelezaji wa miradi mbalimbali inayoibuliwa na halmashauri na mingine ya kitaifa inayotekelezwa katika halmashauri,” amesema Bi. Mwinyimkuu.

Mratibu wa Mafunzo na Mhadhiri Mwandamizi kutoka Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Dkt. Emmanuel Mallya amesema chuo hiki kwa kushirikiana na ofisi ya Waziri mkuu kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji na tathmni nchini hivyo kinaendesha mafunzo haya ili warudipo basi serikali ishuhudie mabadiliko makubwa ambayo yanalenga kuimarisha utendajikazi hasa katika upande wa ufuatiliaji na tathmini.

Mwenyekiti wa washiriki wa mafunzo hayo na Katibu Tawala msaidizi sehemu ya Usimamizi, Ufutiliaji na Ukaguzi kutoka ofisi ya mkuu wa mkoa wa Simiyu, Ndg. Pius Ngaiza, amekipongeza Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kwa kuitendea haki nafasi waliyopewa ya kutoa mafunzo haya kwani wengi walikuwa wanafanya tathmini na ufuatiliaji katika namna ambayo ilileta shida hasa katika ukaguzi, mafunzo haya yamewaimarisha na wanaamini kazi sasa itafanyika kwa kufuata mfumo unaotakiwa kiofisi na hata kitaifa.

Mafunzo haya ni mwendelezo wa mafunzo ya awali yaliyoendeshwa katika jiji la Arusha kanzia Oktoba 7, 2024 hadi Oktoba 11, 2024, ambapo baada ya mafunzo haya yaliyohudhuriwa washiriki 90 kutoka mikoa takriban 13 ambayo kiujumla inakuwa 70% ya halmashauri, manispaa na majiji yote nchini kupata mafunzo haya ya ufuatiliaji na tathmini.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post