PUMA YAAHIDI KUENDELEA NA HUDUMA BORA NA NISHATI SAFI KWA WATANZANIA


Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Mafuta ya Puma Tanzania kupitia Mkurugenzi Mtendaji wake, Fatma Abdallah, amesema mazingira mazuri yaliyowekwa na Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, yameiwezesha kuendelea kutoa huduma bora kwa wateja wake na Watanzania kwa ujumla.

Pia amesema pamoja na kuendelea kutoa huduma bora za viwango vya kimataifa kwa sasa kampuni hiyo imejiwekea mkakati wa kufanikisha malengo ya Rais Samia ya kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

Bi Fatma Abdallah alitoa kauli hiyo leo (Oktoba 9,2024) alipokuwa akizugumza wateja waliofika kıtuo cha mafuta Samnujoma Jijini Dar es Salaam kujaza mafuta. Aidha, wateja hao walipata huduma ya kuoshewa vioo vya gari yao.

Mkurugenzi Mtendaji huyo ameungana na maofisa na wafanyakazi wa Puma kutoa huduma kwa wateja ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha Wiki ya Huduma kwa Wateja Duniani.

Amesisitiza kwamba wanatumia wiki hiyo kuzungumza na wateja na kupata maoni na ushauri wao lengo likiwa kuendelea kutoa huduma bora kila siku, na sio tu katika wiki hii ya maadhimisho ya huduma kwa wateja.

“Katika kuadhimisha wiki ya huduma kwa wateja sisi Puma Energy Tanzania mwaka huu tumeamua kuwa karibu zaidi na wateja wetu , viongozi wote wa Puma Tanzania wako katika vituo vya Tanzania nzima wanahudumia wateja na kuzungumza na wateja na kupata maoni kuhusu huduma zetu na jinsi tunavyoweza kuziboresha zaidi," amesema na kuongeza;

“Tunaamini huduma ambayo Puma Energy Tanzania tunayoitoa tunataka iwe ile ile ambayo mteja anaipata anapokwenda Puma Energy Afrika Kusini au Zambia. Tunataka kuweka ubora uliosawa na wa viwango vya kimataifa duniani kote.”

Ameongeza kwamba wamejipanga vema kutoa huduma bora kwa wateja kwa saa 24 na kuwataka wafanyakazi kujituma.

Pamoja na yote hayo, Bi Fatma Abdallah amesema wameendelea kutoa huduma bora kwa sababu ya mazingira yaliyowekwa na Serikali, kwani yote hayo yasingewezekana kama kusingekuwa na mazingira yaliyobora ambayo Rais Samia ameyaweka kwa wafanyabiashara na Watanzania kufanya biashara kwa urahisi na kwa furaha.

“Katika nchi yetu chini ya uongozi mahiri wa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan wafanyabiashara tumekuwa na mazingira mazuri sana ya kufanyabiashara na sisi Puma Tanzania tumejipanga kutumia mazingira hayo kuendelea kuwahudumia Watanzania.”

Kwa upande wa nishati safi ya kupikia, amesema Puma ni wadau muhimu na tayari wameshaanza programu ya kugawa mitungi ya gesi kwa mama lishe kwa kuanza na Wilaya ya Kigamboni na wataendelea na wilaya zingine za Dar es Salaam na katika mikoa mbalimbali.

“Kampeni ya nishati safi hii ni programu endelevu yenye lengo la kuunga mkono jitihada za Rais Dkt. Samia kuhakikisha tunaenda kutumia nishati safi ya kupikia, mkakati ni kufikia asikimia 80 ya Watanzania ili wapikie nishati safi ifikapo 2034 na sisi Puma Tanzania tuko nyuma kufanikisha mkakati huo na tutaendelea kusambaza mitungi ya gesi ya kupikia majumbani.” Amesema.

Kwa upande wa gesi ya CNG ambayo inatumika katika magari, amesema tayari wanao mkakati mzuri na matatajio yao ni kuwa na vituo ambavyo vitatumika kujaza gesi katika magari kuanzia mapema mwakani.

Kwa upande wa wateja mbalimbali ambao wamehudumiwa na Mkurugenzi huyo wa Puma, Bi Fatma Abdallah wamepongeza Kampuni hiyo kwa kutoa huduma bora za mafuta.

Wamesisitiza kuwa ubora wa huduma zao umekuwa kıvutio kikubwa kwa wateja.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post