RC MWASSA : WAGOMBEA FANYENI KAMPENI ZA KISTAARABU NA ZENYE STAHA



Na Mbuke Shilagi Kagera.

Mkuu wa mkoa wa Kagera hajat Fatma Mwassa amewataka wagombea wote na vyama vya siasa kufanya kampeni za kistaarabu na zenye staha katika uchaguzi wa serikali za mtaa.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo Oktoba 8,2024 amesema kuwa novemba mosi hadi saba wagombea watachukua fomu na kurudisha huku Novemba 20 hadi 26 itakuwa zoezi la kampeni kwa wagombea.

Aidha amesema kuwa mkoa wa Kagera unakadiriwa kuwa na watu wenye umri wa miaka18 na kuendelea wapatao 1,566,530 ambapo amewataka watu wote hao kujitokeza katika zoezi la kupiga kura ili kutumia haki yao ya kimsingi na kikatiba ya kupiga kura na kusema kuwa mkoa wa kagera una vituo vya uandikishaji wa wapiga kura vipatavyo 3,833.

Sambamba na hayo Mkuu wa Mkoa wa Kagera amewakaribisha wananchi wote, makampuni ya uzalishaji wa vyakula, wakulima, wafugaji na wavuvi kushiriki kwa pamoja katika maadhimisho ya chakula duniani.


Amesema kuwa maadhimisho ya siku ya chakula duniani mwaka huu yanaadhimishwa kitaifa katika Mkoa wa Kagera.


Aidha amesema kuwa maadhimisho hayo yatafanyika katika viwanja vya ccm manispaa ya Bukoba kuanzia tarehe 10 -16 octoba 2024 na kuzinduliwa na Mkuu wa Mkoa wa Kagera tarehe 13, na kufungwa na waziri wa kilimo Mh. Hussein Bashe tarehe 16 Oktoba mwaka huu.


Maadhimisho hayo yatakuwa na shughuli mbalimbali ambazo ni mashindano ya mitumbwi ya uvuvi wa samaki, mashindano ya upishi wa asili, ushirikishwaji wa watoto katika unywaji wa maziwa, maonesho ya chakula, burudani,elimu ya uhifadhi wa chakula salama,na udhibiti wa sumu kuvu, Huku yakiambatana na kauli mbiu ya mwaka huu "haki ya chakula kwa wote kwa maisha bora ya sasa na yajao".







Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post