Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

CWT YAWATAKA VIONGOZI WA MATAWI KUSIKILIZA KERO ZA WALIMU



Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Simon Chacha wa pili kushoto,akiwa katika Picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT)Wilaya ya Tunduru na Mkoa wa Ruvuma baada ya kufungua Mkutano Mkuu wa Chama hicho uliofanyika katika ukumbi wa Sky Way Tunduru.
Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma Simon Chacha,akizungumza na Walimu kwenye Mkutano Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania(CWT)Wilayani humo.
Mjumbe wa kamati ya utendaji Taifa ya Chama cha Walimu Tanzania Sabina Lipukila,akizungumza kwenye mkutano Mkuu wa Chama hicho Wilayani Tunduru.
Baadhi ya Walimu wilayani Tunduru,wakimsikiliza Mkuu wa Wilaya hiyo Simon Chacha (hayupo pichani) wakati akifungua mkutano mkuu wa uchaguzi wa Chama cha Walimu Tanzania(CWT)Wilayani humo.

***
Na Regina Ndumbaro-Tunduru. 

 Chama cha Walimu Tanzania (CWT) Mkoani Ruvuma kimewataka viongozi wa matawi katika shule mbalimbali kuhakikisha wanatenga muda wa kusikiliza na kutatua kero za walimu ili kuongeza morali ya kufundisha. 

Wito huo umetolewa na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Taifa wa CWT, Sabina Lipukila, wakati wa Mkutano Mkuu wa uchaguzi wa chama hicho uliofanyika wilayani Tunduru. 

Lipukila amesema baadhi ya viongozi wanashindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo, jambo linalowafanya walimu kukata tamaa na kushuka kwa morali ya kazi.

Lipukila amesisitiza kuwa viongozi wa matawi wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kusimamia haki za walimu na kushughulikia changamoto zao badala ya kuwalazimisha kufuata huduma katika ngazi za juu. 

Ameeleza kuwa baadhi ya walimu wanalazimika kutembea umbali mrefu kufuata huduma ambazo zinaweza kutatuliwa katika ngazi ya shule. 

Ametoa wito kwa viongozi wa CWT kuhakikisha kuwa wanajenga mazingira bora ya kazi kwa walimu ili kuwawezesha kujikita katika ufundishaji.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Simon Chacha, amewataka walimu kuendelea kufanya kazi kwa bidii na weledi ili kuinua kiwango cha elimu wilayani humo. 

Amesema serikali inatambua mchango wa walimu katika maendeleo ya taifa na itaendelea kuwathamini kwa kuhakikisha wanapata mazingira mazuri ya kufundishia. 

Chacha amesisitiza kuwa hakuna taifa lolote lililopiga hatua za maendeleo bila kuwa na walimu bora, hivyo aliwataka walimu kuongeza juhudi ili kuhakikisha wanafunzi wanafaulu kwa viwango vya juu.

Katibu wa CWT Wilaya ya Tunduru, Mtamila Abdul, amebainisha kuwa wilaya hiyo ina jumla ya walimu 1,553, ambapo 1,268 kati yao ni wanachama wa CWT. 

Amesema chama kimekuwa mstari wa mbele katika kuwatetea walimu kwa kuwapatia ushauri wa kisheria na kusaidia wanachama wenye kesi mahakamani. 

Pia, chama kimeshirikiana na serikali kuhakikisha walimu wenye sifa wanapandishwa vyeo na kurekebishiwa mishahara yao, jambo ambalo limeongeza motisha kwa walimu katika utendaji wao wa kazi.

Mtamila ameongeza kuwa CWT imeendelea kusaidia wanachama wake kwa kutoa misaada ya kifedha kwa walimu wenye matatizo mbalimbali. 

Pia, ameipongeza serikali kwa juhudi zake za kuboresha sekta ya elimu, ikiwemo kuajiri walimu wapya na kuwapandisha vyeo walimu waliostahili. 

Amewataka walimu kuendelea kushirikiana na chama hicho ili kuimarisha mshikamano na kuhakikisha changamoto zinazowakabili zinashughulikiwa kwa ufanisi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com