
Evance Kamenge
Na Lydia Lugakila - Kagera
Evance Kamenge, Mkulima na mchumi kutoka Wilaya ya Missenyi, Mkoani Kagera, ametangaza rasmi nia yake ya kugombea nafasi ya ubunge katika Jimbo la Nkenge katika uchaguzi wa mwaka 2025.
Hii ni hatua ya tatu kwake baada ya kushiriki katika uchaguzi wa mwaka 2015 na 2020 bila ya kufanikiwa.
Akizungumza na waandishi wa habari katika Manispaa ya Bukoba, waliotaka kujua masuala mbali mbali yahusuyo siasa ambapo Kamenge amethibitisha kwamba yuko tayari kuwasilisha ombi lake la ridhaa kwa wananchi wa Nkenge.
"Niliwahi kugombea na sasa nataraji kugombea tena mwaka huu 2025," amesema Kamenge.
Kamenge ameeleza kuwa yeye ni sehemu ya mabadiliko na kwamba kuna umuhimu wa kuweka mikakati thabiti ya kuboresha hali ya maisha ya wananchi.
"Mimi ni mkulima na ninaajiri watu, haya ninayoyasema yanatokana na hali halisi ya maisha ya familia yangu kiuchumi," amesema Kamenge.
Mwanasiasa huyo pia amesisitiza kwamba anapokusudia kugombea, anataka kuwa sehemu ya mapinduzi siyo mageuzi.
Amesema kuwa ameona mambo mengi yanapaswa kubadilishwa ili kufikia maendeleo halisi huku akidai kutoridhishwa na hali ya maendeleo katika eneo lake.
Aidha, Kamenge ameonesha kuwa ana imani kwamba viongozi wa sasa wanapaswa kutekeleza ahadi zao huku akiongeza kuwa anatazamia kuwaambia wananchi ukweli huo wakati utakapowadia na yeye akiwa na afya njema.
Kamenge pia amegusia umuhimu wa viongizi kuwa waaminifu katika siasa, akitaja msemo ulioko kwenye kadi yake ya chama chake CCM isemayo "Nitasema kweli daima, fitina kwangu ni mwiko." kauli ambayo imeonesha hali ya kukazia dhamira yake na kueleza haja ya kuwa na viongozi waaminifu na wanaojali maslahi ya wananchi.
Social Plugin